MD Digital

Monday, July 6, 2015

Wanahabari tujitoe kwa mambo yanayotuhusu tuache kutumika



MWANDISHI wa habari ni mtu muhimu sana katika jamii, na wakati mwingine amekuwa akitambulika kama Mhimili wa nne usio rasmi wa serilali, ukiacha Bunge, Mahakama na Serikali.

Waandishi wapo mstari wa mbele sana kuhamasisha jamii kushiriki katika shughuli za maendeleo, kupaza sauti juu ya kero mbalimbali zilizopo katika jamii hizo na hata watatuzi wa hizo kero ama serikali au makundi mengine katika jamii hizo kuona na kutafuta ufumbuzi wake.

Mwandishi wa habari ni mtu ambaye huitumia kalamu yake ama kujenga kitu au mtu na mtu huyo ama kitu hicho kuonekana ni bora zaidi kuliko vyote lakini pia kalamu hiyo hiyo Mwandishi anaweza kuitumia kuboa kabisa kile alichokijenga kwa sifa nyingi na jamii kuona huyu ndio mtu.

Hebu ona sasa hivi mwandishi wa habari hasa Yule anayeaminika katika chumba fulani cha habari alivyo ‘lulu’ katika kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi mkuu wa Rais, Wabunge na madiwani.

Kila mtu mwenye nia ya kutaka kugombea kuwania moja ya nafasi za uongozi anahaha kupata mwandishi ambaye kama si kuamuandika vizuri gazetini au kumtangaza vizuri na hao wapiga kura wake watarajiwa wakamsoma ili wamchague.

Ndio! Na waandishi wa wazuri wapo wengi sasa wadau hapa wanazidiana kete tu na mtu kutoka huku kwenda huku. Wapo wanaofanya kazi hiyo ya kuwapamba na kuwafagilia watu ilimradi tu aione kesho yake bila kujadi maadili au laa  lakini wapo wanaoifanya kazi hiyo kwa kuzingatia maadili.

Mwandishi wa habari amekuwa mbele sana katika kufanya mambo ya watu, lakini akijisahau yeye mwenye matatizo lukuki yanayo mkabili. Hebu angalia wafanyakazi wa kampuni fulani wagome kuhusiana na maslahi duni wanayopata au manyanyaso kwa mwajiri wao uone kesho watakavyo andika magazetini na kutangaza, lakini wamesahau kuwa wao ndio watu wa mwisho katika maslahi na hata hayo madogo wanayotakiwa kuyapata hawayapati kwa wakati.

Hivi sisi waandishi tumelogwa! Na kama ndio basi aliyetuloga hiyo tunguli kaitupa baharini na na mganga mwenye kujua tiba yake kafa. Haiwezekani tumeshindwa kujikingia kifua, ni waoga au nini kinatusibu hata kushindwa kupigania maslahi yetu? Jamani haya maslahi tunashindwa hata kusaidiana nako tunashindwa?

Juzi Kundi fulani la waandishi lisilo rasmi liliamua kuendesha kampeni ya kutafuta fedha za kuwasaidia wenzao wanaumwa maradhi mbalimbali ikiwepo saratani.

Nilifika katika tamasha hilo lililopewa jina la ‘Media Car Wash for Cancer’ pale viwanja vya Leaders  Dar es Salaam nikiwa mshereheshi (MC) na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Said Meck Sadic alikuwa mgeni rasmi, pia tulikuwa na Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Paul Makonda.

Viongozi hao walifika kutunga mkono katika harambee hiyo, mapema akimkaribisha mgeni rasmi Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Paul Makonda alisikitishwa sana na hali za waandishi wa habari jinsi wanavyofanya kazi katika mazingira magumu, wakiwa na maslahi duni pasipo na mikataba ya ajira. Ndio! Wengi wetu tunaishi kama vibarua na hata hao walio ajiriwa au kuwa na mikataba ni duni.

Makonda aliomba ridhaa ya Mkuu wa Mkoa kama vipi alibebe suala la kufuatilia maslahji ya wanahabari kama alivyofanikiwa kwa madereva wan chi hii, ambao leo wamepota mikataba inayoeleweka na mbioni kupatiwa bima za afya wao na familia zao.

Naamini kabisa Makonda sakata la madereva alilijua kupitia waandishi na vyombo vya habari.

Katika harambee hiyo waandishi hawakujitokeza kwa wingi wao kama tunavyojuana idadi yetu. Tumeshindwa kujitokeza kucheza ngoma yetu wenyewe je tumtarajie nani atoke acheze? Sidhani kama Makonda atatosha bila sisi wenyewe kuonesha nia ya kujisaidia.

Licha ya umasikini wetu lakini wengi wetu tuna magari ambayo yangeoshwa pale na kupata fedha, mbona pikipiki yangu Mkuu wa Mkoa na Mkuu wake wa Wilaya waliiosha na kuingiza sh 150,000/=. Wachache waliokuja nawapongeza na waendelee na moyo huo huo, tukijua fika leo kwao kesho kwetu.

Wanahabari wakati umefika sasa wa kila mmoja wetu kujitoa katika mambo yetu na kuacha kutumiwa na watu kwa faida zao. Tumekuwa watumwa wa wanasiasa hivi sasa lakini ngoja washinde kama hata simu au sms yako atajibu. 
Porojo hii imechapishwa kwa mara ya kwanza katika gazeti la Habarileo Julai 05,2015 kama Wazo la Mwandishi.

No comments: