MD Digital

Wednesday, October 9, 2013

MRATIBU MISS UTALII 2013 ADAIWA KUDHALILISHA WASHIRIKI.




Miss utalii Tanzania 2013, Hadija Mswaga (kushoto) akiingia kwenye Uwanja wa ndege wa kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere jijini Dar es Salaam jana, kuelekea Equatorial Guinea kuiwakilisha Tanzania katika mashindano ya Dunia ya Miss Tourisim World 2013, pembeni ni mshindi wa tatu, Teresia Kimolo. aliyemsindikiza (Picha na Hosea Joseph)
BARAZA la Sanaa la Taifa (Basata), limempa karipio kali Mwenyekiti wa shindano la Miss Utalii, Gideon Chipungahelo kwa kosa la kudhalilisha baadhi ya washiriki na malalamiko kufanyiwa kazi na Baraza hilo.
Karipio hilo lilitolewa baada ya Basata kupitia tathmini iliyohusisha vipande vya matukio yaliyorekodiwa (clips) na kujionea namna wasichana wanavyofanyiwa vitendo vya udhalilishaji na Chipungahelo kwa kipindi cha kambi ya miezi mitatu.
Katika hafla ya upitiaji wa clips hizo uliofanyika mwishoni mwa wiki katika Ukumbi wa Basata, Ilala, jijini Dar es Salaam mbele ya Chipungahelo, ilionekana wazi wasichana kukosa uangalizi walipokuwa kambini, hivyo kuwepo kwa matukio mbalimbali yasiyofaa.
Akizungumza katika kikao hicho, Mkuu wa kitengo cha Sanaa wa Basata, Nsao Shaluwa alisema baada ya kupata malalamiko kuwa wasichana wanafanyiwa mambo yasiyofaa wakiwa kambini, waliamua kuutafuta ukweli na kujiridhisha shindano hilo lina ukakasi mwingi.
Alisema baada ya kukusanya baadhi ya matukio katika kuthibitisha hali halisi iliyopo kwenye shindanohilo, watapeleka vielelezo kwa Waziri wa Wizara ya Habari, Vijana Michezo na Utamaduni ili Chipungahelo ajadiliwe kwa kosa la kudhalilisha warembo wa shindano hilo.
Alisema kwa kukosa matroni, yaelezwa warembo walikuwa wakizurula kutwa nzima hadi usiku kwenye gari huku kukiwa hakuna ratiba ya chakula ya kueleweka huku wakifanyishwa mazoezi muda mrefu.
Mbali ya muda mrefu kuanzia saa 2 usiku hadi 9, pia walikuwa wakivaa viatu virefu, hivyo miguu kuvimba na wakati mwingine walikuwa wakichapwa makofi na kulazimishwa mapenzi.
Aidha, Chipungahelo anakabiliwa na shutuma ya kuwaweka mabini washiriki kwa muda wa miezi mitatu tofauti na alivyoeleza Basata kuwa kambi ni ya wiki tatu.
Zaidi ya hapo, Chipungahelo alishindwa kutoa zawadi kwa washindi wala kifuta jasho kwa washiriki wengine huku mshindi wa mwaka 2013, akidaiwa kubebwa kwa hila.
Shaluwa alisema baada ya malalamiko hayo kufikishwa kwao, waliamua kunyatia katika kambi yake iliyokuwa na warembo saba ambayo pia Chipungahelo aliwaficha.
Baada ya kuwahoji washiriki, walikiri kwamba walikuwa wakilala warembo saba, wengine watano katika chumba kimoja na wengine wakilala chini huku wakila mlo mmoja tena katika muda usiofaa.

“Warembo wengi wamekiri walikuwa wakifanyishwa mazoezi kwa muda mrefu huku wakiwa wamevaa viatu virefu,
“Tulikuwa tukifanyishwa mazoezi kuanzia saa mbili usiku hadi saa tisa, tuna njaa na tulipolalamika, baba alitutukana matuzi ya nguoni na kukashifu tupu zetu” mmoja wsa warembo alisema katika CD ya Basata.
Shaluwa anasema walipofika Ikondolelo ambako kulikuwa na kambi ya awali, walizungumza na warembo hao, lakini wakishindwa kusema ukweli mbele ya Chipungahelo.
Alisema walipowapa karatasi kuandika kero zao, kila mtu aliandika jina na kusaini ambapo walieleza mengi yaliyorekodiwa na wadau kuoneshwa mwishoni mwa wiki mbele ya mwanasheria Ashura Mzava kutoka TAWLA.
Mzava alisema wazi kwa madudu yaliyopo kwenye shindano hilo, Chipungahelo anapaswa kushtakiwa kwa udhalilishaji.
Kashfa nyingine ni kitendo cha Chipungahelo kutumia kiasi cha sh 200,000 ambazo zilitolewa na Mkuu wa Wilaya Tanga Mjini, Halima Dendego ili washiriki waende saloon kabla ya fainali.
“Baba ametunyanyasa sana hadi, ametumia pesa tuliyopewa na mama Halima Dendego, lakini hapohapo amekuwa akimpendelea mshiriki mwenzetu (jina tunalo), kwa vile alikuwa na uhusiano naye wa kimapenzi,” alisema mmoja wa washiriki na kuongeza:
“Hata siku ile ya fainali, alipokuja mpambaji kutoka Sofia Record, alimuita na kumvalisha nguo nzuri pamoja na kumpamba tofauti na alivyovalisha washiriki wengine” wamesema washiriki hao.
Wakati huohuo Mkurugenzi Msaidizi wa Sanaa kutoka Wizarani, Leah Kihimbi alisema atalifikisha kwa usahihi suala hilo katika ngazi ya juu akimtaka Chipungahelo ajitayarishe kwa maamuzi yoyote.
Mshiriki pekee wa Miss Utalii 2013 aliyefika kwenye tahmini hiyo, ni Glory John aliyesema wazi shutuma zote zilizoelezwa na wenzake dhidi ya Cipungahelo ni kweli.
“Tulipokuwa tunakwenda Mikumi , tulilala Morogoro, Baba (Chipungahelo) aliniita akaniambia nipande juu katika chumba kimojawapo, nilipokwenda na kufungua mlango, nikakutana na moshi wa ajabu nikashindwa kuvumilia nikatoka.
Akanifuata akinitaka nirudi chmbani mle, nikagoma, nilipowaeleza wenzangu, walinieleza nilielekea kunaswa kwenye mtego wake,” alisema Glory.
Naye Katibu Mtendaji BASATA Godfrey Mngereza alisema, hilo ni suala nyeti linalogusa jinsia ya kike, hivyo ni hatari kwa ustawi wa jamii.
Kupitia tathmini hiyo ya aina yake, Basata itachunguza mazingira ya ushindi wa Miss Utalii mwaka 2013, ikibainika hakustahili, atavuliwa taji hilo ili iwe fundisho.
“Tabia hizi chafu zinatuchafua hata sisi BASATA tunaonekana hatufanyi kazi sasa ndio tutaanza na Miss Utalii na ikibidi kusiwe na shindano la aina yeyote kama mambo yenyewe ni kudhalilishana,” alisema Mngereza.
Wadau wengine waliohudhuria tathmini hiyo ni kutoka TAMWA, TAWLA,TGNP,THAWE, Polisi Jamii, Polisi kutoka kituo cha Pangani Ilala, Dar es Salaam, Shirikisho la Sanaa na Ufundi, Binti Leo na wengineo.

Shaluwa alisema suala hilo litapelekwa ngazi za juu na vielelezo kuonesha wasichana wakieleza yanayotokea kambini pamoja na maoni ya wadau yaliyorekodiwa.
Akizungumnzia tuhuma dhidi yake, Chipungahelo alisema ni majungu yaliyopikwa na maadui zake ambao walimpandikizia makahaba kwa lengo la kuchafua taswira ya shindano hilo ili kummaliza, lakini aliomba radhi kwa dosari na mapungufu yaliyojitokeza na kuahidi kuwa hazitajirudia tena.

Tuesday, October 8, 2013

TBL Yazindua mashindano ya mitindo na ubunifu nchini

Meneja masoko wa TBL Fimbo Butallah akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar Es Salaam kwenye uzinduzi wa mashindano ya ubunifu na mitindo kwa wanafunzi wa vyuo vya elimu ya juu nchini ( Redd's Uni-Fashion Bash 2013) yatakayofanyika katika mikoa ya Dar Es Salaam,Mwanza,Iringa na Kilimanjaro.Kushoto ni Meneja mawasiliano na habari wa Tbl Edith Mushi.
*******
Na Mwandishi Wetu
KAMPUNI ya Bia Tanzania (TBL) kupitia kinywaji chake cha Redd’s Original imezindua tamasha la mitindo na ubunifu kwa wanafunzi wa vyuo vya elimu ya juu hapa nchini, litakalojulikana kama ‘Redd’s Uni-Fashion Bash’.

Akizungumza katika uzinduzi huo uliofanyika Dar es Salaam jana, Meneja Masoko wa TBL, Fimbo Butallah alisema,  tamasha hilo lenye lengo la kuinua vipaji vya wanafunzi katika tasnia ya mitindo, linatarajiwa kuanza mwezi huu na kumalizika mwezi ujao.

Butallah alisema, tamasha hilo kwa sasa litashirikisha vyuo vyote vya elimu ya juu vilivyopo katika Mikoa ya Dar es Salaam, Iringa, Kilimanjaro na Mwanza.

“Tunataka kuinua vipaji vya wanafunzi wa vyuo katika tasnia ya mitindo, kupitia maonyesho yakatakayofanywa na wanafunzi wa vyuo hivyo, hapa tunataka wale wenye ubunifu kuonyesha ubunifu wao wa mitindo, hivyo hii ni fursa kwao kujitangaza na kudhihirisha uwezo wao,” alisema Butallah.

Kuhusu ushiriki, Butallah alisema, kutakuwa na fomu maalumu zitakazosambazwa katika vyuo husika, ambapo wanafunzi wanamitindo na wabunifu watazijaza na majaji watazipitia na kupata wabunifu 10 na wanamitindo wa idadi hiyo kutoka kila mkoa, ambao watapata fursa ya kuonesha mavazi yao siku ya tamasha.

Kuhusu zawadi, Meneja Habari na Mawasiliano wa TBL, Edith Mushi alisema, kutakuwa na zawadi mbalimbali kutoka Redd’s Original, ambapo washindi watano wa ubunifu na idadi kama hiyo ya wanamitindo kutoka kila mkoa watajiondokea na fedha taslimu.

Edith alisema, kwa upande wa wabunifu mshindi wa kwanza ataondoka na Sh 700,000 wa pili Sh 500,000 watatu Sh 300,000 huku wa nne na watano kila mmoja akiondoka na Sh 100,000.

Kwa upande wa wanamitindo mshindi wa kwanza atajiondokea na Sh 500,000 wa pili Sh 400,000 wa tatu Sh 300,000 wakati wanne na watano wakipata Sh 100,000 kila mmoja.

“Tuna imani kubwa zawadi hizi zitaongeza chachu kwa wabunifu na wanamitindo kuendeleza fani hii ya mitindo. Lakini matamasha haya pia yatahusisha burudani za aina mbalimbali za kuvutia.

“Hii itakuwa sehemu muhimu ya kuwakutanisha wanafunzi wa vyuo na kada mbalimbali katika kufurahia na kubadilishana mawazo juu ya masuala ya ubunifu na mitindo, kwani kinywaji cha Redd’s Original kimekuwa mstari wa mbele katika kuendeleza tasnia ya urembo, ubunifu na mitindo hapa nchini,” alisema Edith.

Kinywaji cha Redd’s Original pia ndicho kinachodhamini shindano la Redd’s Miss Tanzania na kinazalishwa na kusambazwa na Kampuni ya Bia Tanzania (TBL).

Thursday, April 5, 2012

Wednesday, September 21, 2011

Mti wa Matunda unapochanwa Mbao

Wakazi waKipera wakichana mbao mti waMzambarau kijijini hapo.

KUNDI LA T-MOTO MODERN TAARAB LATUA DAR KUFYATUA SITA MPYA KWA MPIGO

KUNDI jipya la muziki wa taarab la Tanzania Moto Modern Taarab (T-Moto) limetua jijini Dar es Salaam leo asubuhi kutoka mfichoni katika Visiwa vya Zanzibar, lililokuwa limejichimbia kwa ajili ya maandalizi ya uzinduzi wake uliosogezwa mbele hadi Oktoba 28 mwaka huu.
Kundi hilo limewasili jijini baada ya kusitisha mazozi yake kwa muda kwa ajili ya maombolezo ya msiba wa Meli ya Mv Spice na linatarajia kuingia studio kwa ajili ya kurekodi nyimbo zake mbili kati ya zilizosalia ili kukamilisha albamu yao.
Akizungumza katika Bandari ya jijini Dar es Salaam jana, Mkurugenzi wa kundi hilo Amin Salmin, alisema kwamba kundi hilo litaingia katika stuio za Bakunde na kurekodi nyimbo sita ambazo zitakamilisha albamu yao iitwayo ‘Aliyeniumba Hajanikosea’.
Aidha alisema kuwa baada ya kumaliza zoezi la kurekodi nyimbo hizo, kundi hilo linatarajiwa kufanya ziara katika mikoa ya Tanzania na nchi jirani ya Kenya, kabla ya kufanya uzinduzi rasmi wa kundi na albamu yao Oktoba 28, jijini Dar es Salaam.
Mmoja wa wasanii wa kundi hilo ambaye ni mkongwe katika muziki huo wa Taarab, Bi. Mwanahawa Ally alisema anashukuru kambi hiyo imewaweka katika mwelekeo mzuri ambapo anaamini kazi zitakazotoka zitakuwa na viwango vya hali ya juu hivyo amewaomba mashabiki wakae mkao wa kula.
“Nataka niwaeleze mashabiki wa tasnia ya taarab kwamba tunakuja kwa moto kama lilivyo jina la kundi letu, moto ambao si rahisi kuzimika kwa kijipipa cha maji, hivyo mashabiki wetu wasubiri mambo mazuri na ya kupendeza kutoka kwetu, tunawaomba mashabiki watupokee vizuri kwa kujitokeza kwa wingi katika maonyesho yetu,”Alisema.
Tayari kundi hilo limeshatoa nyimbo mbili ambazo zimeweza kuliwatambulisha vyema.
Nyimbo hizo ni pamoja na uliobeba albamu hiyo‘ Aliyeniumba Hajanikosea’ ulioimbwa na Mwanahawa Ally, pamoja na ‘Unavyojidhani Mbona Hufanani’ ulioimbwa na Jokha Kassim.
Nyimbo nyingine zinazotarajiwa kuwamo katika albamu hiyo ni pamoja na ‘Mtoto wa Bongo’ ulioimbwa na Hassan Ally, ‘Mchimba Kaburi Sasa Zamu yake imefika’ ulioimbwa na Mrisho Rajab, ‘ Mwenye Kustiri Mungu’, ‘Kumbe Wewe ni Shoti’ ambazo zimeimbwa na Mosi Suleiman na ule wa ‘ Riziki na Shortcut’ ulioimbwa na Aisha Masanja.
Kundi hilo limesheheni wasanii wenye vipaji vya hali ya juu wakiwemo Mwanahawa Ally, Jokha KAssim, Jumanne Ulaya ‘Mkono wa Biashara’, Mrisho Rajab, Musa Mipango, Hassan Ally, Mosi Suleiman, Rajab Kondo, Fadhili Mnara, Moshi Mtambo, Ally Kabura, Sabha, Rahma , Asha Masanja na Hanifah Kasim na wengineo.